SALAAM ZA MWAKA MPYA ZA RAIS KIKWETE KWA WANANCHI

SALAAM ZA MWAKA MPYA ZA RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA,
MHESHIMIWA JAKAYA MRISHO KIKWETE KWA WANANCHI, TAREHE 31 DESEMBA, 2012

Utangulizi
Ndugu zangu, Watanzania Wenzangu;
Ni furaha na faraja kubwa kuifikia siku hii adhimu ya kuuaga mwaka wa
2012 na kuukaribisha mwaka 2013. Ni jambo la bahati ambayo hatuna budi
kumshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehma, kwa kutujaalia uzima na
kutuwezesha kuumaliza mwaka huu salama. Wapo ndugu, jamaa na marafiki
zetu wengi ambao wangependa kuiona siku hii lakini hawakujaaliwa.
Wametangulia mbele ya haki. Tuendelee kuwaombea kwa Mwenyezi Mungu
awape mapumziko mema. Amin. Nasi tumuombe Mola wetu atujaalie
fanaka tele katika mwaka ujao.
Mapitio ya Mwaka 2012
Ndugu wananchi;
Mwaka tunaoumaliza leo ulikuwa wenye mambo mengi mazuri na mafanikio
makubwa, lakini, pia, ulikuwa na changamoto zake. Baadhi zilikuwa
ngumu na zipo zilizokuwa za kusikitisha na kuhuzunisha.
Ajali za barabarani na majini ziliendelea kupoteza maisha ya watu
wengi na kusababisha majeraha na ulemavu kwa maelfu. Ajali mbaya
kuliko zote kutokea, mwaka huu, ilikuwa ile ya meli ya MV Skagit
iliyotokea tarehe 18 Julai, 2012 ambapo watu 144 walipoteza maisha.
Ajali za barabarani zilizosababisha vifo nazo ziliongezeka kutoka
3,012 mwaka 2011 hadi kufikia 3,144 na kusababisha vifo vya ndugu zetu
3,714.
Ndugu Wananchi;
Kufuatia ajali ya MV Skagit ambayo ilitokea miezi 11 baada ya ile ya
MV Spice Islander, Serikali zetu mbili zimekuwa zikishirikiana kwa
karibu kuhusu masuala ya usafiri wa majini kati ya Tanzania Bara na
Zanzibar. Kwa ajili hiyo SUMATRA na Zanzibar Maritime Authority
zinafanya kazi kwa karibu zaidi na kanuni za usafirishaji wa abiria na
mizigo na za usajili na ubora wa meli zimewianishwa. Ni matumaini
yetu kuwa hatua hizo zitasaidia kumaliza ajali zinazotokana na makosa
ya wanadamu.
Ndugu Wananchi;
Kwa upande wa ajali za barabarani tuliendelea na tutaendelea
kuwahimiza madereva kuheshimu Sheria za Usalama Barabarani, waepuke
uzembe na hasa ulevi wakati wa kuendesha. Tutaendelea kuwakumbusha
wenye magari kuhakikisha kuwa uzima wa magari yao unakuwa wa kiwango
cha juu. Hali kadhalika, tumewataka Polisi waongeze ukali na kuwabana
ipasavyo madereva na wamiliki wa magari ili watekeleze wajibu wao na
wasipofanya hivyo wawajibishwe inavyostahili.
Hali ya Usalama
Ndugu wananchi;
Tunaumaliza mwaka huu nchi yetu ikiwa shwari, salama na tulivu.
Tuombe Mungu hali hii iendelee mwaka 2013 na idumu milele. Mipaka ya
nchi yetu ipo salama na uhusiano na majirani na nchi zote duniani ni
mzuri. Tunaendelea kutafuta suluhu ya mgogoro wa mpaka kati ya nchi
yetu na Malawi katika Ziwa Nyasa kwa njia ya mazungumzo. Suala hilo
limewasilishwa kwa pamoja na Serikali zote mbili kwa Mheshimiwa
Joaquim Chissano, Mwenyekiti wa Umoja wa Viongozi Wastaafu wa Afrika
kwa ajili kuzisaidia nchi zetu kupata ufumbuzi. Matumaini yetu ni
kuwa viongozi hao watalishughulikia suala hili mapema iwezekanavyo.
Ushirikiano wa Kanda
Ndugu Wananchi;
Ushirikiano wetu wa kikanda katika Jumuiya ya Afrika Mashariki na
katika Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika (SADC) unaendelea
vizuri. Mwaka huu nchi yetu imepewa heshima kubwa ya kuwa Mwenyekiti
wa Chombo cha SADC kinachoshughulikia masuala ya Siasa, Ulinzi na
Usalama.
Jukumu hilo ni zito na hasa katika kipindi hiki ambapo kuna
changamoto za kisiasa na kiusalama katika nchi za Jamhuri ya
Kidemokrasia ya Kongo, Madagascar na Zimbabwe. Nchi yetu inatarajiwa
kuongoza juhudi za kupata ufumbuzi wa migogoro hiyo migumu. Ndiyo
maana tulifanya Mkutano Maalum wa Wakuu wa Nchi za SADC hapa Dar es
Salaam tarehe 7 na 8 Desemba, 2012. Mwaka ujao, kwa kushirikiana na
wenzetu, tutaendeleza juhudi zetu. Ni matumaini yangu kuwa tukipata
ushirikiano wa viongozi na wananchi wa nchi husika na jumuiya ya
kimataifa tutapata ufumbuzi tunaotaka.
Ndugu Wananchi;
Kwa upande wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, tumeendelea kushuhudia
Jumuiya hiyo na harakati za utangamano zikizidi kustawi. Jengo la
Makao Makuu ya Jumuiya limekamilika na kuzinduliwa rasmi tarehe 28
Novemba, 2012. Siku hiyo hiyo kule Athi River, Kenya, barabara ya
kutoka Arusha hadi Athi River ilizinduliwa. Barabara hii ni moja ya
miradi kadhaa inayotekelezwa kwa pamoja na nchi wanachama wa Jumuiya
wa Afrika Mashariki.
Mchakato wa utangamano wa kiuchumi wa Afrika Mashariki unaendelea kwa
kasi. Tanzania ikiwa sehemu kamili ya mchakato huo, lazima
tuhakikishe kuwa tunakwenda nao sambamba. Tusikubali kuachwa nyuma
wala kuwa chanzo cha kuuchelewesha mchakato huo bila ya sababu za
msingi. Utangamano una maslahi kwa nchi yetu na manufaa yake ni
makubwa. Kwa mfano, mauzo yetu katika soka la Afrika Mashariki
yameongezeka sana kutoka dola za Kimarekani milioni 58.6 mwaka 2000
hadi kufikia dola za Kimarekani milioni 409 mwaka 2011.
Jumuiya imekuwa kichocheo muhimu cha kukuza uzalishaji, ajira na
uchumi hapa nchini. Kwa ukubwa wa nchi yetu na rasilimali tulizonazo
tuna matumaini makubwa ya kunufaika zaidi siku za usoni. Naweza
kuthubutu hata kusema kuwa Tanzania inaweza kunufaika zaidi kuliko
nchi nyingine wanachama wa Jumuiya hiyo. Kinachotakiwa ni sisi
kujipanga vizuri kwa sera na mipango ili tuzitumie fursa tulizonazo
kwa maslahi ya uchumi na maendeleo ya nchi yetu na watu wake. Tuache
woga, tujiamini.
Matishio ya Usalama
Ndugu Wananchi;
Licha ya kumaliza mwaka nchi ikiwa shwari na yenye amani na utulivu,
yalikuwepo matukio yaliyotishia usalama wetu. Bahati mbaya na kwa
masikitiko makubwa matukio hayo yalisababishwa na baadhi ya viongozi
wa dini na siasa na wafuasi wao. Kwa kweli kwa mara ya kwanza nchi
yetu ilifikishwa kwenye hatari ya kutokea mgawanyiko mkubwa wa
Watanzania au hata mapigano ya raia kwa misingi ya dini zao. Bahati
nzuri hilo halikutokea na Mungu aliepushe lisitokee kamwe.
Nimeshalisemea jambo hili siku za nyuma na napenda kurudia tena leo
kuwasihi Watanzania wenzangu kupima athari za kauli zetu na matendo
yetu kwa mustakabali wa jamii yetu, nchi yetu na watu wake. Viongozi
wa dini, waumini na viongozi wa siasa na wafuasi wao wanao wajibu
maalum wa kuhakikisha kuwa Watanzania wanaendelea kuishi kwa upendo,
amani na ushirikiano bila kujali tofauti ya dini zao, makabila yao,
rangi zao au maeneo watokako. Hiyo ndiyo sifa ya nchi yetu tunayoijua
sote ambayo ni njema na watu wengi wanataka kuja kujifunza kwetu na
wale wenye shida wanatamani wawe kama sisi. Hii ni tunu muhimu ya
taifa ambayo tusikubali kuipoteza kwa maslahi binafsi ya watu
wachache.
Ndugu Wananchi;
Wakati wo wote, lazima tutambue umuhimu wa kuvumiliana na kuheshimiana
kwa tofauti zetu za kidini, rangi, kabila, tutokako na ufuasi wa vyama
vya siasa. Lazima pia tuhakikishe kuwa tunaheshimu sheria na
taratibu zinazotawala mikutano na maandamano. Tukiyazingatia hayo
nchi yetu itakuwa haina tishio lo lote kwa amani na usalama wake.
Yasipozingatiwa tunaiweka nchi yetu hatarini. Sisi katika Serikali
tutakuwa hatuna la kufanya bali kutimiza wajibu wetu wa kulinda
usalama wa raia na nchi yetu. Wahusika watachukuliwa hatua na vyombo
vya usalama na kisheria kwa mujibu wa sheria za nchi. Tulifanya hivyo
mwaka huu na hatutakuwa na ajizi kufanya hivyo siku yo yote kama
hapana budi.
Uhalifu Unapungua
Ndugu Wananchi;
Inatia moyo kuona kuwa mwaka huu makosa ya jinai yalipungua na
kufikia 66,255 yakilinganishwa na makosa 69,678 ya mwaka jana au
94,390 ya mwaka juzi. Hii inathibitisha kuimarika kwa kazi nzuri
inayofanywa na Jeshi la Polisi wakishirikiana na wananchi na vyombo
vingine vya usalama. Pamoja na hayo lazima tuongeze juhudi za
kupambana na uhalifu kwani bado matukio ni mengi mno na upungufu bado
ni mdogo. Tutaendeleza kazi tuifanyayo sasa ya kuliimarisha Jeshi la
Polisi kwa rasilimali watu, zana na vitendea kazi husika.
Uhalifu wa Kimtandao
Ndugu Wananchi;
Tutaongeza nguvu katika kupambana na uhalifu unaoendeshwa na mitandao
ya uhalifu ndani na nje ya nchi. Mitandao hiyo hasa imekuwa
inajihusisha na biashara ya kusafirisha wanadamu, biashara ya dawa za
kulevya na biashara ya nyara za Serikali.
Mapambano dhidi ya uhalifu wa kimtandao yametuwezesha kukamata
wahamiaji haramu 4,765 na tayari 1,611 wamerudishwa kwao. Kwa upande
wa dawa za kulevya watuhumiwa 6,929 walikamatwa mwaka huu
ukilinganisha na 209 mwaka 2011. Kilo 55,285 za dawa za kulevya
zilikamatwa mwaka huu ukilinganisha na kilo 17,752.4 mwaka jana. Kwa
upande wa nyara za Serikali, zilizokamatwa ni 1,416 na kati ya hizo
736 ni meno ya tembo. Watuhumiwa 1,037 walikamatwa na kesi 746 zipo
Mahakamani katika hatua mbalimbali.
Ndugu Wananchi;
Taarifa hizi zinathibitisha kuimarika kwa jitihada za kupambana na
uhalifu wa kimtandao. Tutaimarisha zaidi jitihada zetu mwaka 2013 ili
tupate mafanikio zaidi. Tutaviongezea uwezo wa rasilimali watu, zana,
vifaa na fedha za uendeshaji vyombo vyetu vya usalama vinavyoongoza
mapambano haya.
Tutaimarisha na kuendeleza ushirikiano baina ya nchi yetu na nchi
jirani na nyinginezo duniani. Hii itasaidia kutuongezea uwezo wa
kupambana na mitandao ya uhalifu ndani ya nchi, kikanda na kimataifa.
Pia tutazipitia upya sheria za kupambana na makosa haya kwa nia ya
kuziboresha.
Ndugu Wananchi;
Katika mwaka 2013, tutapanua na kuimarisha huduma ya matibabu kwa watu
walioathirika na dawa za kulevya kote nchini. Tutakamilisha ujenzi wa
kituo cha Dodoma na kujenga kingine kipya Dar es Salaam. Natoa wito
kwa wale wote walioathirika au watu wenye watoto au rafiki au jamaa
walioathirika waende hospitali kupatiwa matibabu kwani matibabu hayo
ni bure.
Hali ya Uchumi
Ndugu wananchi;
Katika mwaka 2012, tunaoumaliza leo, uchumi wa nchi yetu uliendelea
kukua na kuimarika licha ya kuwepo kwa changamoto za upatikanaji wa
umeme, kupanda kwa bei za mafuta na chakula duniani na uhaba wa mvua
katika maeneo mengi nchini uliosababisha kupungua kwa uzalishaji na
kupanda kwa bei za vyakula nchini. Pia, licha ya kuendelea kwa
msukosuko wa uchumi wa dunia na hasa katika Bara la Ulaya ambako ni
soko kuu la bidhaa zetu na watalii. Mategemeo yetu ni kuwa, mwaka
huu, uchumi wetu utakua kwa asilimia 6.8 na mwakani (2013) utakua kwa
asilimia 7.0 ukilinganisha na asilimia 6.4 mwaka 2011.
Kwa jumla, ukilinganisha na makadirio ya IMF ya kiwango cha ukuaji wa
uchumi wa dunia kuwa asilimia 3.3 mwaka huu, ni dhahiri kuwa uchumi
wetu unakua kwa kasi nzuri na kuifanya Tanzania iendelee kuwa miongoni
mwa nchi ambazo uchumi wake unakua kwa kasi kubwa.
Hali hii ya uchumi wetu ina maana kubwa mbili. Kwanza, kwamba uchumi
wetu umejenga uhimilivu dhidi ya misukosuko ya uchumi wa dunia. Na
pili, kwamba shughuli za uzalishaji na huduma zinazidi kukua na mauzo
ya bidhaa ndani na nje ya nchi yameongezeka. Kuongezeka kwa mauzo ya
nje kumefanya akiba yetu ya fedha za kigeni kufikia dola za Marekani
bilioni 3.9 mwezi Novemba, 2012 kiasi ambacho kinatuwezesha kuagiza
bidhaa kutoka nje kwa miezi minne.
Ndugu Wananchi;
Makusanyo ya mapato ya Serikali yatokanayo na kodi yalifikia shilingi
bilioni 580.3 mwezi Oktoba, 2012 ikilinganishwa na shilingi bilioni
479.3 mwezi Oktoba 2011. Matarajio yetu ni kufanya vizuri zaidi mwaka
2013 kwa mapato yatokanayo na kodi na yale yasiyotokana na kodi ambayo
bado ni chini ya lengo.
Ndugu Wananchi;
Mfumuko wa bei kuwa juu ni changamoto ambayo tunaendelea kuikabili ili
kuleta utulivu uliokamilifu kwa uchumi wetu na kuwapunguzia ukali wa
maisha wananchi wa Tanzania. Serikali imechukua hatua kadhaa
kudhibiti hali hiyo na mafanikio ya kututia moyo yameanza kuonekana.
Kwa mfano, mfumuko wa bei umepungua kutoka asilimia 19.8 mwezi Desemba
2011 hadi asilimia 12.1 mwezi Novemba, 2012. Kiwango hicho bado ni
cha juu na hakikubaliki. Tutaendelea kuchukua hatua zaidi ili tuweze
kufikia lengo letu la mfumuko wa bei kuwa chini ya asilimia 10 ifikapo
mwezi Juni, 2013.
Miongoni mwa mambo tuliyopanga kufanya ili kupunguza mfumuko wa bei ni
kuimarisha hali ya upatikanaji wa umeme na kudhibiti mwenendo wa bei
ya mafuta. Kufanya hivyo kutasaidia kupunguza gharama za uzalishaji
na uchukuzi wa bidhaa. Aidha, tutaendelea kutekeleza mipango na
mikakati ya kukuza na kuboresha kilimo nchini kwa lengo la
kujihakikishia usalama wa chakula, kukuza pato la taifa na kupunguza
umaskini hasa miongoni mwa wakulima.
Utekelezaji wa Miradi ya Maendeleo
Ndugu wananchi;
Mwaka huu tunaoumaliza leo ulikuwa na mafanikio ya kutia moyo kwa
upande wa utekelezaji wa miradi ya kuendeleza miundombinu nchini.
Tumeshuhudia miradi ya barabara, madaraja, viwanja vya ndege, reli,
bandari, umeme na maji ikikamilika, au kuanzwa au utekelezaji wake
ukiwa unaendelea. Hakika lengo la kuunganisha mikoa yote ya Tanzania
Bara kwa barabara za lami siyo ndoto tena bali ni jambo la uhakika na
litatimia muda si mrefu ujao.
Ndugu Wananchi;
Kwa upande wa reli, mwaka huu tumeendelea kukarabati reli ya kati na
kurejesha usafiri wa treni kutoka Dar es Salaam kwenda Mwanza na
Kigoma. Mwaka ujao (2013) tutaendeleza kazi ya ukarabati wa reli hiyo
muhimu na kuzidi kuboresha huduma. Tumekamilisha ujenzi wa viwanja
vya ndege vya Mpanda na Songwe na tunaendelea kuboresha viwanja vya
Tabora, Kigoma, Bukoba, Mafia, Mwanza na Zanzibar. Tumeendelea
kujenga na kupanua miundombinu ya maji nchini na kuboresha upatikanaji
wa maji salama kwa Watanzania. Kwa mwaka huu usambazaji wa maji salama
umefikia asilimia 87 kwa watu wa mijini na asilimia 61.5 vijijini.
Tutaendeleza kazi hiyo mwaka 2013.

Msongamano wa Magari Dar es Salaam
Ndugu Wananchi;
Katika Jiji la Dar es Salaam tumeendelea na tutaendelea kuchukua hatua
mbalimbali za kupunguza msongamano wa magari unaozidi kuongezeka.
Barabara mpya zimejengwa na zinaendelea kujengwa ndani na kuzunguka
Jiji. Barabara kadhaa zimepanuliwa na nyingine zitaendelea
kupanuliwa. Ujenzi wa miundombinu (barabara na vituo) ya mabasi
yaendayo haraka umeanza. Mwaka 2013 ujenzi wa barabara za juu ya
nyingine katika makutano ya TAZARA utaanza na matayarisho ya kufanya
hivyo kwa makutano ya Ubungo yatakamilishwa.
Tumetimiza ahadi yetu ya kutumia treni kusafirisha abiria katika jiji
la Dar es Salaam. Usafirishaji umeanza na unaendelea kati ya Stesheni
na Ubungo na kutoka Stesheni ya TAZARA hadi Pugu – Mwakanga. Mwaka
ujao tutaendelea kuimarisha usafiri huo kwa kuongeza treni na idadi ya
safari. Tayari Mshauri Mwelekezi ameshateuliwa kufanya upembuzi
yakinifu na kushauri kuhusu kupanua huduma hiyo mpaka ifike Tegeta,
Bunju, Kimara, Luguruni, Kibaha, Mbagala-Rangi Tatu na Kongowe.
Ushauri huo pia utahusu kuwa na huduma bora ya usafiri wa treni katika
Jiji la Dar es Salaam kwa maana ya aina ya njia, vichwa vya treni na
mabehewa. Tuliamua kuanza na reli na treni iliyopo, lakini nia yetu
ni kufanya vile hasa inavyotakiwa iwe kwa usafiri wa treni mijini.
Umeme
Ndugu Wananchi;
Mwaka tunaoumaliza leo haukuwa rahisi kwa upande wa upatikanaji wa
umeme. Mabwawa ya kuzalisha umeme ya Kidatu, Kihansi, Mtera, Pangani
na Nyumba ya Mungu yameendelea kutokuwa na maji ya kutosha kwa sababu
ya uhaba wa mvua. Hivyo basi taifa limelazimika kutegemea umeme wa
kukodi unaozalishwa kwa kutumia mafuta. Umeme huo umekuwa wa gharama
kubwa na hivyo kuwa mzigo mkubwa kwa TANESCO na taifa. Serikali
imeendelea kushirikiana na TANESCO na kuisaidia kubeba mzigo huo.
Tutaendelea kufanya hivyo mwaka ujao na mpaka tutakapofikia hatua ya
kutokuwa na ulazima wa kutumia umeme wa kukodi.
Ndugu Wananchi;
Mtakumbuka kuwa tulipopata tatizo la ukame na upungufu wa umeme mwaka
2006/2007, Serikali yetu iliazimia kuongeza uzalishaji wa umeme
kutokana na vyanzo vingine vikiwemo gesi asili, makaa ya mawe, upepo
na jua. Nafurahi kusema kuwa, tangu wakati ule Serikali imeiwezesha
TANESCO kujenga vituo vitatu vinavyozalisha MW 245 kwa kutumia gesi.
Hatukuweza kuongeza zaidi uzalishaji wa umeme kwa kutumia gesi kwa
sababu ya kiasi cha gesi kinacholetwa Dar es Salaam kutoka Songo Songo
kuwa kidogo. Ndiyo maana tukaamua kujenga bomba jipya kubwa la
kusafirisha gesi kutoka Songo Songo hadi Dar es Salaam.
Ndugu Wananchi;
Kwa nia ya kutaka kuhakikisha kuwa kutakuwa na gesi ya kutosha
kuzalisha umeme mwingi zaidi pale inapohitajika, ikaamuliwa bomba hilo
liendelezwe mpaka visima vya gesi vya Mtwara. Ujenzi wa bomba hilo
umeanza mwezi Novemba, 2012 na unatarajiwa kukamilika ndani ya miezi
18. Gesi itakayopatikana ina uwezo wa kuzalisha MW 3,000 za umeme.
Tayari mipango inaendelea ya kujenga mitambo ya kuzalisha MW 900 pale
Kinyerezi ili mara gesi itakapofika umeme uzalishwe. Hatua hiyo
itatuwezesha kuung’oa mzizi wa fitina wa mgao wa umeme na mzigo wa
kununua umeme ulio ghali.
Utafutaji wa Gesi
Ndugu Wananchi;
Tangu mwaka 2010 gesi nyingi imegundulika baharini na nchi kavu
katika Mikoa ya Mtwara, Lindi na Pwani. Utafutaji bado unaendelea na
tuna matumaini kuwa gesi nyingi zaidi huenda ikagundulika. Hivi sasa
Serikali inaandaa sera na sheria mpya ya gesi ili kuboresha
zinazotumika wakati huu. Nia yetu ni kutaka kuhakikisha kuwa
rasilimali hii adhimu inasimamiwa vizuri kwa manufaa ya nchi yetu na
watu wake pamoja na kulinda maslahi ya wawekezaji.
Napenda kutumia nafasi hii kuwahakikishia ndugu zetu wa kule gesi
ilipogunduliwa au popote itakapogundulika, kuwa watanufaika sawia na
katu hawatasahaulika. Rai yao ya kutaka na wao wanufaike inakubalika
na Serikali inajiandaa hivyo. Viongozi wa Mikoa ya Lindi na Mtwara kwa
mfano, wanajua maelekezo niliyotoa kuhusu kuiandaa miji ya Mtwara na
Lindi kupokea uchumi wa gesi.
Lakini, sharti la kutaka gesi isisafirishwe kwenda kokote na kwamba
kila kitu kifanyike kwao halikubaliki. Rasilimali inayopatikana po
pote katika nchi hii ni mali ya taifa zima na hutumika kwa manufaa ya
taifa. Katu siyo mali ya watu wa pale ilipogundulika au pale shughuli
hizo zinapofanyika. Jumla ya makusanyo ya mapato yatokayo sehemu zote
za nchi yetu na kutokana na vyanzo mbalimbali ndiyo yanayotumika
kuhudumia watu wote po pote walipo.
Ndugu Wananchi;
Huu ni msingi mzuri, ni sera nzuri na ni jambo jema la tunu,
tulilorithi kwa waasisi wa Taifa letu, ambalo hatuna budi kulienzi na
kulidumisha. Nawasihi wanasiasa wenzangu tusiwaelekeze kwenye mambo
mabaya wananchi tunaodai kuwapenda. Kutafuta umaarufu kwa agenda
zinazopandikiza chuki kwa watu na kuligawa au kulibomoa taifa, ni
upungufu mkubwa wa uongozi na uzalendo. Tuache siasa za ubarakara na
kuwapa watu matumaini yasiyotekelezeka. Nawaomba wananchi
msiwasikilize, si watu wanaowatakia mema na wala hawaitakii mema nchi
yetu.
Elimu
Ndugu wananchi;
Tumeendelea kupata mafanikio katika utekelezaji wa sera yetu ya
kupanua fursa ya elimu kwa Watanzania katika ngazi zote. Mwaka huu
vijana wetu wengi zaidi walijiunga na elimu ya msingi, sekondari,
ufundi na elimu ya juu. Hivi sasa tunaelekeza juhudi zetu zaidi
katika kuongeza ubora wa elimu. Kwa ajili hiyo, tumechukua hatua za
makusudi za kupanua mafunzo na ajira za walimu wa shule za msingi na
sekondari. Kwa mfano, mwaka huu walimu 24,621 wapya waliajiriwa kati
yao 11,379 wa shule za msingi na 13,242 wa shule za sekondari.
Januari, 2013 tunategemea kuajiri walimu 28,746 kati yao 14,606 wa
shule za msingi na 14,060 watakuwa wa shule za sekondari.
Kwa sababu hiyo, uwiano wa mwalimu kwa wanafunzi umeendelea kuwa
mzuri. Hivi sasa kwa shule za msingi uwiano umefikia 1:46
ukilinganisha na 1:56 mwaka 2005. Uwiano unaostahili ni 1:40. Kwa
upande wa sekondari uwiano wa mwalimu kwa wanafunzi hivi sasa ni 1:29
ukilinganisha na 1:20 unaostahili. Kutokana na upanuzi wa vyuo vya
kufundisha walimu nchini, bila ya shaka baada ya miaka mitatu hivi
upungufu wa walimu wa shule za msingi na sekondari haitakuwa kilio
tena.
Ndugu Wananchi;
Upatikanaji wa vitabu nao unazidi kuwa bora. Hivi sasa uwiano wa
kitabu kwa mwanafunzi ni 1:3 kwa shule ya msingi na sekondari 1:3
ukilinganisha na 1:5 kwa shule za msingi na sekondari 1:4 mwaka 2009.
Hata hivyo, tutaendelea kuongeza mgao wa fedha katika bajeti ya elimu
ili kuongeza upatikanaji wa vitabu na vifaa vingine vya kusomea na
kufundishia. Tunataka katika muda mfupi ujao uwiano uwe 1:1.
Kwa upande wa maabara za sayansi, tarehe 4 Novemba, 2012, nilipokuwa
kwenye ziara ya Mkoa wa Singida, nilitoa agizo la kutaka ndani ya
miaka miwili, kuanzia mwaka 2013, kila shule ya sekondari ya kata
nchini iwe na majengo ya maabara yaliyokamilika. Yawe pia yanatumika
kwa maana ya vifaa na mahitaji muhimu. Nimewataka Wakuu wa Mikoa na
Wilaya kuhakikisha kuwa agizo hili linatekelezwa kwa ukamilifu.
Kuanzia sasa, katika ziara zitakazofanywa Mikoani na mimi, Makamu wa
Rais na Waziri Mkuu tutapenda kupata taarifa ya maendeleo ya
utekelezaji wake.
Ndugu Wananchi;
Kwa upande wa ufundishaji imedhihirika kwamba mkakati maalum
unahitajika kuboresha ufundishaji wa masomo ya hisabati, kiingereza na
sayansi katika shule za msingi na sekondari. Matokeo ya mitihani ya
darasa la saba na kidato cha nne kwa miaka mingi sasa yanathibitisha
haja hii. Sasa wakati umefika kwa suala hili kulipa uzito
unaostahili. Tutafanya hivyo kuanzia mwaka 2013.
Afya
Ndugu Wananchi;
Mwaka 2012 ulikuwa na mafanikio mengi ya kutia moyo kwa upande wa
sekta ya afya nchini pamoja na kuwepo kwa changamoto mbalimbali. Kazi
ya kusogeza huduma ya afya karibu na wanapoishi watu kwa maana ya
kujenga zahanati, vituo vya afya, hospitali mpya na kuimarisha
zilizopo iliendelea kutekelezwa kwa mafanikio kote nchini.
Hali kadhalika, uwezo wetu wa ndani wa uchunguzi na tiba ya magonjwa
makubwa umezidi kuimarika mwaka huu. Upatikanaji wa dawa, vifaa vya
uchunguzi na vifaa tiba umeendelea kuboreshwa. Aidha, mafunzo na
ajira za madaktari, wauguzi na wataalamu wengine wa afya vimeendelea
kuongezwa. Kituo cha Tiba ya Maradhi ya Moyo kimekamilika katika
Hospitali ya Taifa ya Muhimbili na mwaka ujao (2013) shughuli za
upasuaji na nyinginezo husika kutibu maradhi ya moyo zitakuwa
zimeboreshwa sana. Upanuzi mkubwa wa Hospitali ya Saratani ya Ocean
Road umekamilika. Kwa ajili hiyo, huduma zitakuwa bora zaidi na
msongamano wa wagonjwa hospitalini hapo utakuwa umemalizika. Ujenzi
wa hospitali kubwa ya kisasa katika Chuo Kikuu cha Dodoma unaendelea
vizuri na inatarajiwa kukamilika mwaka 2014. Hospitali hiyo itatumika
kufundishia wanafunzi wa udaktari na uuguzi.

Ndugu Wananchi;
Mwaka huu pia, tumekamilisha matayarisho ya kuanza ujenzi wa
hospitali kubwa na ya kisasa kabisa kule Mlonganzila, Dar es Salaam.
Ujenzi utaanza Februari 2013 na kukamilika Februari, 2015. Hospitali
hii pia itakuwa ya kufundishia wakati Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi
Shirikishi cha Muhimbili kitakapohamishia sehemu kubwa ya shughuli
zake huko Mloganzila. Mchakato wa ujenzi wa Chuo hicho nao unakaribia
kuanza. Kuwepo kwa hospitali hizi kutaongeza sana uwezo wetu wa ndani
wa uchunguzi na tiba. Sasa naweza kuthubutu kusema kuwa safari ya
kupunguza wagonjwa tunawaopeleka nje tumeianza kwa dhati.
Ndugu Wananchi;
Tumeendelea kupata mafanikio katika mapambano dhidi ya magonjwa
makubwa yanayosababisha vifo vingi kama vile UKIMWI, Kifua Kikuu na
Malaria. Maambukizi na vifo vinazidi kupungua. Pia vifo vya kina
mama na watoto vinaendelea kupungua.
Kwa mujibu wa taarifa za mwaka huu za Shirika la Afya Duniani, vifo
vya watoto wenye umri chini ya miaka mitano hapa Tanzania vimepungua
kutoka vifo 81 kwa kila watoto 1000 waliozaliwa hai mwaka 2009 hadi
kufika vifo 65.2 mwaka 2011 na vifo vya watoto wachanga vimepungua
kutoka vifo 51 kwa kila watoto 1000 waliozaliwa hai mwaka 2009 na
kufikia vifo 45 mwaka 2011. Mafanikio haya yanaiweka Tanzania katika
orodha ya nchi 10 zinazofanya vizuri duniani katika kupunguza vifo vya
watoto wenye umri wa chini ya miaka mitano.
Ndugu Wananchi;
Hatuna budi kufahamu kuwa haya ni matokeo ya kufanya vizuri kwenye
chanjo kwa watoto ambayo imefikia wastani wa asilimia 90. Pia
imechangiwa na mafanikio yetu katika kupunguza maambukizi ya malaria
na UKIMWI kwa watoto. Naamini tutapata mafanikio makubwa zaidi
kuanzia mwaka 2013 tutakapoanza chanjo dhidi ya kichomi (pneumonia) na
ugonjwa wa kuharisha kwa watoto chini ya umri wa miaka mitano. Aidha,
tukiendelea kutekeleza kwa dhati mpango wa kila mtoto kulala kwenye
chandarua kilichotiwa dawa na ule Mpango Kabambe wa Kuzuia Maambukizi
ya Mama Kwenda kwa Mtoto niliouzindua kule Lindi tarehe 1 Desemba,
2012, mambo yatakuwa vizuri zaidi.
Sensa ya Watu na Makazi
Ndugu wananchi;

Leo asubuhi kwenye viwanja vya Mnazi Mmoja nilitangaza matokea ya
Sensa ya Watu na Makazi iliyofanyika mwezi Agosti, mwaka 2012.
Matokeo haya yanaonyesha kwamba idadi ya watu nchini Tanzania ni
milioni 44,929,002 kati yao watu milioni 43,625,434 wanaishi Tanzania
Bara na milioni 1,303,568 wanaishi Zanzibar. Ukilinganisha na Sensa
ya mwaka 2002 tulipokuwa na watu milioni 34.4, hili ni ongezeko la
watu milioni 10.5 au wastani wa asilimia 2.6 kwa mwaka.
Matokeo haya yana maana kubwa kwa Serikali na kwa kila mmoja wetu.
Kwa kasi hii ya ongezeko la watu ifikapo mwaka 2016 Tanzania itakuwa
na watu milioni 51.6. Hii ni idadi kubwa sana ya watu inayoleta
changamoto kwa Serikali na jamii. Hatuna budi kutambua maana ya idadi
hiyo ya watu na kujipanga vyema kukidhi mahitaji yao na hasa
kuhakikisha kuwa maskini hawaongezeki na huduma zinatosheleza mahitaji
na zina ubora wa juu. Kazi hiyo lazima ianze sasa na ionekane katika
Mipango ya Maendeleo.
Ndugu Wananchi;
Kwa upande wetu, sisi wananchi, taarifa hii inamlazimu kila mmoja wetu
atambue kuwa kwa kasi hii, siku za usoni nchi yetu itakuwa na watu
wengi, hivyo ushindani kwa rasilimali utakuwa mkubwa. Watakaofanikiwa
wakati huo ni wale wenye familia ndogo au zile ambazo zimepanga uzazi.
Tukipanga uzazi tunajipa nafasi ya kutunza na kulea vizuri watoto
wetu na kuwapatia mahitaji yao muhimu ya maisha.

Ndugu Wananchi;
Napenda kutumia nafasi hii kurudia kuwashukuru wananchi wenzangu wote
kwa ushirikiano wenu uliowezesha zoezi zima kufanikiwa kiasi hiki.
Aidha, nawashukuru kwa dhati viongozi, watendaji wakuu na maofisa wote
waliopanga, kuratibu, kusimamia na kutekeleza zoezi la kuhesabu watu.
Natoa shukrani maalum kwa Kamati ya Kitaifa ya Sensa, Kamati za Sensa
za Mikoa na Wilaya, Ofisi ya Taifa ya Takwimu ya Jamhuri ya Muungano
na Afisi ya Mtakwimu Mkuu wa Zanzibar na makarani wote wa sensa.
Penye nia pana njia. Tumeweza kushinda changamoto zote na kuwapatia
Watanzania nyenzo muhimu ya kupanga mipango ya maendeleo yao.
Vitambulisho vya Taifa
Ndugu wananchi;
Mwaka huu tumeanza zoezi la kusajili watu na makazi kwa ajili ya
kuandaa kutoa Vitambulisho vya Taifa kuanzia mwaka 2013. Mamlaka ya
Vitambulisho vya Taifa ilifanya zoezi la majaribio katika mkoa wa Dar
es Salaam na wilaya ya Kilombero ambalo lilifanikiwa. Hivi sasa
wanaendelea na zoezi hilo Zanzibar. Maandalizi kwa ajili ya kutekeleza
zoezi la kutoa vitambulisho nchi nzima kuanzia mwaka 2013 yanakwenda
vizuri. Napenda kuwasihi wananchi wenzangu wakati utakapofika kutoa
ushirikiano unaostahili kwa maafisa watakaohusika na kukusanya taarifa
na kutoa vitambulisho ili zoezi lifanikiwe ipasavyo. Nawaomba
muitumie vizuri fursa hii ya kujisajili na kupata vitambulisho.
Mchakato wa Katiba Mpya
Ndugu wananchi;
Mtakumbuka kuwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba nililiyoiunda tarehe 1
Mei, 2012 ilianza kazi yake rasmi tarehe 29 Juni, 2012 na inaendelea
vyema. Mpaka sasa Tume imekamilisha hatua ya kwanza ya kukusanya
maoni ya mtu mmoja mmoja katika Mikoa yote nchini. Napenda kuchukua
nafasi hii kuwashukuru wananchi kwa kujitokeza kwa wingi kutoa maoni.
Zoezi linalofuata ni la kukusanya maoni ya makundi maalumu kuanzia
mwezi Januari, 2013. Natoa wito kwa makundi hayo nayo kushiriki
vizuri kwenye hatua hii muhimu. Baada ya hatua hiyo kukamilika, Tume
itaandaa Rasimu ya Katiba ambayo wanategemea itakuwa tayari mwezi Mei,
2013.
Ndugu Wananchi;
Kwa mujibu wa ratiba ya Tume, rasimu hiyo itawasilishwa kwenye Vikao
vya Mabaraza ya Katiba vitakavyofanyika kati ya mwezi Juni na Agosti,
2013. Tume itatangaza muundo na namna ya kuwapata Wajumbe wa
Mabaraza hayo na utaratibu utakaotumika wakati wa kujadili na kutoa
maoni juu ya Rasimu ya Katiba wakati huo ukiwadia.
Baada ya kukamilika kwa Vikao vya Mabaraza ya Katiba, Tume
itakamilisha Rasimu ya Katiba ambayo itachapishwa kwenye Gazeti la
Serikali kama yalivyo matakwa ya Sheria. Aidha, itachapishwa katika
magazeti ya kawaida kwa wananchi kusoma. Mwezi Novemba, 2013 rasimu
hiyo itawasilishwa kwenye Bunge Maalum kujadiliwa na kupitishwa.
Baada ya Bunge Maalum kupitisha Rasimu ya Katiba, Rasimu hiyo
itapelekwa kwa wananchi kwa uamuzi wa mwisho kupitia kura ya maoni.
Ndugu Wananchi;
Matarajio yetu ni kwamba kama kila kitu kitakwenda kama
inavyotarajiwa nchi yetu itakuwa na Katiba Mpya iliyotokana na maoni
na matakwa ya wananchi ifikapo mwaka 2014. Mwaka huo Muungano wetu
utakuwa unatimiza miaka 50 hivyo hiyo itakuwa zawadi ya tunu kubwa.
Tukifanikiwa kupata Katiba mpya wakati huo, tutafanya Uchaguzi Mkuu wa
mwaka 2015 kwa kutumia Katiba hiyo. Inshallah, Mwenyezi Mungu
atajaalia baraka zake, nia yetu njema itatimia. Pamoja na hayo, natoa
wito kwenu wananchi wenzangu kushiriki kwa ukamilifu katika hatua zote
za mchakato ili tuweze kujenga muafaka kuhusu Katiba tunayoitaka.

Marekebisho ya Sheria
Ndugu Wananchi;
Katika hotuba yangu ya mwisho wa mwezi wa Februari, 2012, nilieleza
kwamba katika mazungumzo baina ya Serikali na vyama vya siasa na
wadau wengine juu ya marekebisho ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba
tulikubaliana tushughulikie marekebisho ya Sheria hiyo hatua kwa
hatua. Tulikubaliana kuanza na mambo yanayohusu Tume ya Kuratibu na
Kukusanya Maoni ya Wananchi ili Tume iundwe na ianze kazi. Baada ya
hapo tuangalie vipengele vinavyohusu Bunge Maalum na Kura ya Maoni.
Tulifanya hivyo kuhusu Tume ya Katiba na sasa tunajiandaa kuanza
mazungumzo kuhusu ngwe iliyobaki yaani, Bunge Maalum na Kura ya Maoni.
Kama mazungumzo yatakamilika mapema kunako Januari, 2013 mapendekezo
hayo yatafikishwa katika Bunge la Jamhuri ya Muungano katika kikao cha
Februari kwa uamuzi. Vinginevyo itakuwa katika Bunge la Aprili,
2013.
Ndugu Wananchi;
Kuhusu Kura ya Maoni, Sheria ya Mabadiliko ya Katiba inaelekeza kuwa
Kura ya Maoni itatungiwa Sheria yake maalum. Ni matumaini yangu kuwa
matayarisho yake yataanza mapema iwezekanavyo. Nawasihi wananchi
wenzangu, viongozi wa vyama vya siasa na asasi za kijamii tuwe
watulivu, tuendelee kushirikiana katika mchakato huu wa Katiba mpaka
tulifikishe jahazi ufukweni salama kwa mustakabali mwema wa nchi yetu
na watu wake.
Mfumo wa Dijitali
Ndugu wananchi;
Bila ya shaka mtakumbuka taarifa za Wizara ya Mawasiliano, Sayansi na
Teknolojia na Tume ya Mawasiliano kwamba kuanzia tarehe 1 Januari,
2013 nchi yetu itahamia katika mfumo wa mawasiliano unaotumia
teknolojia ya dijitali (au kidijiti kwa tafsiri ya BAKITA) badala ya
huu wa sasa wa analojia. Uamuzi huu unakuja kufuatia uamuzi wa
kimataifa kwamba nchi zote duniani ziwe zimeingia kwenye mfumo huu
ifikapo mwaka 2015. Pia unazingatia uamuzi wa Jumuiya ya Afrika
Mashariki kwa nchi zetu kuanza safari hiyo tarehe 1 Januari, 2013.
Hapa nchini zoezi hili litafanyika kwa awamu. Litaanza katika mikoa
saba ya Dar es Salaam, Arusha, Dodoma, Mbeya, Kilimanjaro, Mwanza na
Tanga na mingine itafuata kwa mujibu wa ratiba itakayopangwa.
Ndugu Wananchi;
Teknolojia ya dijitali katika mfumo wa mawasiliano hufanya picha za
televisheni kuwa nzuri na hazina chenga chenga. Mawasiliano ya simu
yatakuwa mazuri zaidi. Vile vile, itakuwa rahisi kupata huduma za
televisheni kwenye simu za mkononi na huduma ya intaneti kwenye
televisheni.
Ndugu Wananchi;
Ili kuweza kutumia teknolojia hii, kila televisheni inatakiwa iwe na
kifaa kiitwacho king’amuzi. Vifaa hivi vipo kwa wingi madukani na
wengine tayari wanavyo. Naomba niwatoe hofu kwamba kwa kuingia katika
mfumo huu siyo lazima kununua televisheni mpya. Televisheni yo yote
yenye vitundu vitatu vya rangi za njano, nyeupe na nyekundu itaweza
kufanya kazi kwenye mfumo wa dijitali. Hata wale ambao hawana
televisheni za namna hiyo wanaweza kununua kifaa cha kuunganishia
king’amuzi na mambo yakawa mazuri.
Uhusiano wa Kimataifa
Ndugu wananchi;
Katika mwaka 2012, uhusiano wetu na washirika wetu wa maendeleo
ulikuwa mzuri na uliendelea kuimarika. Wote wanaridhika na kusifu
kazi nzuri inayofanywa na Serikali yetu na ndiyo maana wanaendelea
kushirikiana nasi na kutoa misaada ya maendeleo. Aidha, wameonesha
nia thabiti ya kuendelea kushirikiana nasi na kutusaidia katika
harakati zetu za kujiletea maendeleo.
Napenda kutumia nafasi hii kwa niaba yenu nyote kutoa shukrani za
dhati kwa washirika wetu wa maendeleo kwa mchango mkubwa wanaoendelea
kutoa kwa maendeleo ya nchi yetu. Nawahakikishia kuwa tunathamini
sana ushirikiano wao na misaada yao na tutafanya kila tuwezalo
kudumisha ushirikiano baina yetu.
Mkutano wa Smart Parntership
Ndugu Wananchi;
Mwaka huu nchi yetu ilipata bahati ya kuwa mwenyeji wa mikutano
mikubwa ya kikanda na kimataifa. Mikutano hiyo ni pamoja na Mkutano
Mkuu wa Shirika la Mapinduzi ya Kijani Afrika (AGRA), Mkutano wa Mwaka
wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB), Mkutano Mkuu wa Shirika la
Kimataifa la Chanjo (GAVI) na Mkutano wa Wakuu wa Nchi za SADC.
Bahati nzuri mwaka 2013 Tanzania itakuwa mwenyeji wa mikutano mingine
ukiwemo ule wa Global 2013 Smart Partnership Dialogue utakaofanyika
Dar es Salaam kuanzia tarehe 24 – 28 Mei, 2013. Huu ni mkutano
unaohusisha nchi nyingi duniani na kutoka takriban mabara yote.
Mkutano huu hukutanisha na kushirikisha viongozi wa Serikali wakiwemo
Wakuu wa Nchi na Serikali, viongozi wa sekta binafsi wakiwemo wa
makampuni makubwa ya kimataifa, wasomi na wawakilishi wa asasi za
kiraia na watu binafsi.
Kwa kawaida katika mkutano kama huu huwepo agenda maalum, aghalabu
kuhusu masuala ya uchumi, biashara na maendeleo. Mkutano wa mwaka
2013 utazungumzia “Matumizi ya Sayansi na Teknolojia kwa Ajili ya
Maendeleo ya Afrika” (Leveraging Science and Technology for Africa’s
Development). Kwa kweli ni kipaumbele muafaka kabisa, ndiyo maana na
sisi tumefarijika kuukaribisha.

Ndugu Wananchi;
Kuwa mwenyeji wa mkutano mkubwa kama huu wa watu zaidi ya 500
mashuhuri, ni heshima kubwa kwa nchi yetu. Ni nafasi nzuri ya
kuitangaza Tanzania na fursa zake za uwekezaji, biashara na utalii.
Pia, ni nafasi nzuri kwa wafanyabiashara wetu kutangaza shughuli zao
na fursa za biashara na uwekezaji wanazotaka kushirikisha
wafanyabiashara wa nje. Naomba tuitumie vyema fursa hiyo adimu kwa
manufaa ya taifa na ya waanyabiashara wetu. Tuwaonyeshe wageni wetu
upendo na ukarimu kama ilivyo sifa yetu Watanzania ili waondoke na
kumbukumbu nzuri za nchi yetu na watamani kurudi tena kutembea au
kuwekeza.
Hitimisho
Ndugu wananchi;
Tunatarajia kuwa mwaka 2013 utakuwa mwaka wa mafanikio makubwa zaidi
katika nyanja zote kuzidi mwaka 2012. Mambo yaliyokwama mwaka 2012
yatakwamuliwa. Ajira zitaongezeka kwa uwekezaji vitega uchumi
kuongezeka na kuwajengea uwezo wajasiriamali wazalendo, ili waweze
kujiajiri wenyewe na kuajiri wengine. Kwa ajili hiyo, Mifuko ya
kusaidia wajasiriamali wadogo, wanawake na vijana itafufuliwa na
kutengewa fedha nyingi katika bajeti ya Serikali.
Mwaka 2013 ni mwaka wa matumaini, hivyo kila mmoja wetu anatakiwa
kujituma na kutimiza wajibu wake. Maisha bora yatakuja kwa kila mmoja
wetu kutimiza wajibu wake ipasavyo. Kama kila mtu atafanya kazi kwa
bidii na maarifa, na, kama kila mmoja wetu atajivunia matokeo ya kazi
yake na siyo uhodari wa maneno yake ya uchambuzi wa hali. Kila mtu
achukie uvivu na tabia ya kulalamika pasipo kufanya kazi.
Ndugu Wananchi;
Mimi na wenzangu Serikalini tunawaahidi ushirikiano wa hali ya juu na
kwamba tutawatumikia kwa moyo wetu wote, kwa nguvu zetu zote na kwa
maarifa yetu yote. Tunataka kukidhi matarajio na imani ya wananchi
kwa Serikali yao. Tutaendelea kuimarisha utendaji kazi Serikalini na
kuhimiza uwajibikaji katika ngazi zote za uongozi. Tutaendeleza
mapambano dhidi ya rushwa bila ajizi na watumishi wasio waaminifu,
wazembe, wabadhirifu wa mali ya umma watawajibishwa ipasavyo.
Wananchi pia wanao wajibu wa kuwa raia wema na wazalendo wa kweli kwa
nchi yao. Kila mmoja wetu ajiulize ataifanyia nini jamii yake na nchi
yake badala ya kuuliza itamfanyia nini.
Ndugu zangu,Watanzania Wenzangu;
Nawatakieni nyote heri na fanaka tele katika mwaka mpya wa 2013.
Tusherehekee pamoja kwa amani na utulivu.

Mungu Ibariki Afrika!
Mungu Ibariki Tanzania!
Asanteni sana kwa kunisikiliza.